Januari 28, 2026 ilihitimishwa rasmi Kambi Maalum ya Huduma ya Kutatua Kero za Wananchi iliyofanyika katika Kata ya Kiriba, Wilaya ya Musoma. Mgeni rasmi katika hitimisho hilo alikuwa Mheshimiwa Juma Chikoka, Mkuu wa Wilaya ya Musoma, ambaye alifunga rasmi kambi hiyo baada ya kukamilika kwa zoezi la siku tatu. Katika hitimisho hilo, Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya alitembelea mabanda yote ya huduma na kupokea taarifa za mwenendo wa utoaji huduma, aina ya kero zilizoshughulikiwa pamoja na idadi ya wananchi waliohudumiwa katika kipindi chote cha kambi.
Akitoa taarifa ya jumla kuanzia siku ya kwanza hadi hitimisho, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, Ndg. Alade Maluli, alisema kuwa kambi hiyo imefanikiwa kwa kiwango kikubwa kutokana na ushirikiano mzuri kati ya wananchi, taasisi za Serikali na uongozi wa Halmashauri. Alibainisha kuwa wananchi walijitokeza kwa wingi kupata huduma mbalimbali na kuwasilisha kero zao, hali inayoonesha imani ya wananchi kwa Serikali yao.
Aidha, alieleza kuwa kero zote zilizopokelewa zimefanyiwa kazi kwa mujibu wa taratibu, huku zile zinazohitaji ufuatiliaji wa muda mrefu zikiwekwa katika mpango maalum wa utekelezaji. Ndg. Maluli alitoa shukrani kwa Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Musoma, viongozi wa kisiasa na kiutendaji, pamoja na watumishi wote walioshiriki, kwa mchango wao katika kuhakikisha kambi hiyo inawafikia wananchi na kuimarisha uwajibikaji wa Serikali
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Halmashauri ya Wilaya ya Musoma (Suguti - Kwikonero, Barabara ya Majita) | 31117 - MUSOMA.
Sanduku la Posta: P.o. Box 344 Musoma
Simu: 0282622163
simu ya mkononi:
Barua pepe: ded@musomadc.go.tz
Hatimiliki@2017 Halmashauri ya Wilaya ya Musoma. Haki zote zimehifadhiwa